Na Gladness Mallya
SAKATA la kijana Bonny Fabian Kavishe kudaiwa kumuua kwa kumpiga risasi
baba yake, mzee Livingstone Kavishe akiamini ni mwizi sasa ni simulizi
ya machozi kufuatia kusomwa kwa waraka mzito ulioandikwa na mtuhumiwa
huyo ambaye bado yupo mahabusu ya Polisi Mlandizi, Bagamoyo, Pwani.
Waraka huo ulizidi kuwatoa machozi baadhi ya waombolezaji siku ya
mazishi yaliyofanyika Marangu, Wilaya ya Moshi Vijijini, Mkoa wa
Kilimanjaro kutokana na maneno yenye huruma ya Bonny kuomba msamaha.
WARAKA ULIANDIKIWA NDANI YA MAHABUSU
Habari zisizo na chenga wala
kumulika tochi zinasema, mtuhumiwa akiwa mahabusu aliamua kuandika
waraka huo na kumpa ndugu yake mmoja (jina halikupatikana) akimpa
maelekezo kwamba usomwe siku ya mazishi ya mzee huyo kabla hajafukiwa
kaburini kwa vile yeye hatakuwepo.
“Kwa kweli inauma sana! Jamaa
alipoona hatapata ruhusa ya askari ili akashiriki mazishi ya baba yake
aliomba karatasi na kalamu na kuandika waraka, akampa ndugu yake mmoja,
akamwambia usomwe siku ya mazishi ya marehemu kabla hajafukiwa
kaburini,” kilisema chanzo.
MWILI WAAGWA NYUMBANI KWA MTUHUMIWA, WASAFIRISHWA NA WARAKA
Jumatano ya Mei 15, mwaka huu, mwili wa marehemu mzee Kavishe uliagwa
nyumbani kwa mtuhumiwa licha ya yeye kutokuwepo na ukasafirishwa kwenda
Marangu kwa mazishi.
Miongoni mwa mambo yaliyozingatiwa kwenye
kusafirisha mwili huo ni uwepo wa waraka huo ambao mtuhumiwa aliomba
usomwe mbele ya waombolezaji siku ya mazishi.
MANENO NDANI WARAKA NI HAYA
Siku ya mazishi, mwanaume aliyepewa
jukumu la kuongea kwa niaba ya familia aliusoma waraka huo huku
waombolezaji wakiwa makini kumsikiliza.
Alisema waraka huo
umeandikwa kwa mikono ya Bonny Kavishe, licha ya kuzungumzia mambo
mengine, aliwaomba msamaha ndugu, jamaa na marafiki kwamba wamsamehe kwa
kitendo cha kumuua baba yake.
Alisema alifanya kitendo hicho bila
kukusudia na wala hajui nini kiliendelea. Haikuwa nia yake kumtoa uhai
baba yake aliyefikia nyumbani kwake Mlandizi kwa ajili ya kusherehekea
harusi ya mdogo wa mtuhumiwa huyo iliyofanyika Mei 11, mwaka huu.
WARAKA WAWATOA MACHOZI WAOMBOLEZAJI
Chanzo kinasema: Yaani wakati
waraka huo ukisomwa ndugu na jamaa walilia sana ikawa ni machozi mara
mbili. Kwanza kwa mzee Kavishe kufariki dunia, pili kwa sababu ya ndugu
yao huyo ambaye yuko mahabusu kutokana na kumuua baba yake. Sehemu kubwa
ya waraka huo, Bonny alikuwa akiomba msamaha.
MTUHUMIWA AFUNGA KULA NA KUNYWA
Maneno mengine yaliyopatikana
ndani ya waraka huo ni mtuhumiwa kusema tangu siku ya tukio hilo, Mei
12, mwaka huu ambapo alikamatwa na kuswekwa mahabusu, hakula wala kunywa
kitu chochote kwa muda wa saa 48 kwa sababu akili yake ilikinai kufuata
utaratibu wa kibinadamu kufuatia kitendo cha kumtoa uhai baba yake.
TUMEFIKAJE HAPA?
Mzee Kavishe alitoka Marangu mkoani Kilimanjaro
na kufika Mlandizi kwa ajili ya harusi ya mtoto wake ambaye ni mdogo wa
Bonny, aitwaye Boniface Fabian Kavishe.
Baada ya harusi kumalizika,
familia ilirudi nyumbani kwa Bonny kwa ajili ya kupumzika. Marehemu
aliandaliwa chumba chake ambapo aliingia kulala huku akiwatakia usiku
mwema wanaye.
Usiku wa saa tisa kuelekea Jumapili, mzee Kavishe
aliamka, akatoka kwenda chooni. Alipomaliza alirudi ndani lakini kwa
vile macho yake yalikuwa hayaoni vizuri alishindwa kutambua chumba
alichokuwa amelala hivyo akajikuta akiingia chumba alicholala mwanaye
Bonny na mkewe Eva.
Inadaiwa wakati huo Eva alikuwa macho, ila Bonny
alikuwa usingizini. Eva alishtuka kusikia kitasa cha mlango kikishikwa
na mtu kuingia, akapiga kelele za mwiziii! Mwizii jamani!
Kelele
hizo zilimwamsha Bonny ambaye naye bila kujua, alichukua bastola kutoka
kwenye makazi yake na kumfyatulia ‘mwizi’ huyo. Risasi ilichomoka kwa
kasi na kumwingia mzee huyo kwenye paji la uso ambapo alianguka chini na
kukata roho papohapo.
Baada ya tukio hilo Bonny alitoka kitandani
na kwenda kuwasha taa kwa lengo la kumtambua ‘mwizi’ huyo. Hamadi! Kumbe
ni baba yake ambaye muda mfupi nyuma walikuwa kwenye cherekochereko za
harusi wakila na kunywa kwa furaha.
MKUU WA KITUO AMWELEZEA MTUHUMIWA
Paparazi wetu alipata nafasi ya
kuzungumza na Mkuu wa Kituo cha Mlandizi, Bagamoyo, Pwani, Afande
Shaban Musa ambapo alikiri kutokea kwa tukio hilo, akasema uchunguzi
bado unaendelea na mtuhumiwa mpaka juzi Jumapili anashikiliwa na jeshi
hilo.
Akaongeza: Hili kweli ni jambo la kuhuzunisha kwani mtuhumiwa
si mtu wa shari, mpole sana lakini nilishangaa siku hiyo kumwona
anakimbilia hapa kituoni mwenyewe na kusema amemuua baba yake.”
Marehemu Kavishe alizikwa Mei 17, 2013.
Mungu ailaze pema peponi rojho yake. Amina.