Na Patrick Mabula, Kahama
HUU
ni ukatili kwa 100%! Martha Charles (22), mkazi wa Nyahanga wilayani
hapa ambaye ni mtumishi wa Halmashauri ya Mji wa Kahama ameuawa kinyama
kwa kuchinjwa shingoni na mume wake, Amani lina habari ya kusikitisha.
Kaimu
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Afande Onesmo Lyanga alisema
tukio hilo lilitokea katikati ya wiki iliyopita ambapo pia alimtaja mume
anayedaiwa kutekeleza unyama huo kuwa ni Asack Nzolela (29),
mfanyabiashara wa bucha la nyama ya ng’ombe.
Afande Lyanga alisema
mtuhumiwa alimchinja mkewe wakiwa wamelala chumbani kwenye nyumba ya
wazazi wa mwanaume huyo na baada ya kufanya ukatili huo alikimbia.
Habari
za uhakika zilizopatikana kutoka katika familia ya marehemu zilisema
chanzo cha mauaji hayo ni ugomvi wa kifamilia ambapo mtuhumiwa alianza
kwa kumlaumu mama yake mzazi kwa kitendo cha kumtafutia kazi mkewe
katika Halmashauri ya Mji wa Kahama wakati yeye alikuwa hataki mkewe
afanye kazi.
Habari zilizopatikana eneo la tukio kutoka kwa mmoja wa
ndugu anayeishi na familia hiyo, Paul Edward alisema mbali na kuchinjwa
shingoni pia marehemu alikatwakatwa sehemu mbalimbali za mwili wake.
Edward
alisema usiku wa tukio akiwa amelala katika moja ya chumba ndani ya
nyumba hiyo, alisikia kelele za ugomvi kutoka kwenye chumba cha wanandoa
hao hali iliyomfanya apige kelele zilizowafikia majirani ambao walifika
kutoa msaada.
Akasema majirani hao sanjari na yeye walimkuta mtuhumiwa ameshamchinja mkewe kwa kisu na kutoweka kusikojulikana.
Nao
majirani waliokwenda kutoa msaada ambao hawakupenda majina yao yatajwe
gazetini, walisema walikuta mwili wa Martha ukiwa kitandani huku
amekatwa na kitu chenye ncha kali katika eneo lote la shingo, ndipo
walipomchukua na kumkimbiza hospitali lakini tayari alikuwa ameshakata
roho.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa, Noel Mkisi alisema baada ya muuaji huyo kutoroka usiku huohuo jitihada za kumsaka zilianza.
Tukio
la kuchinjwa kinyama kwa mwanamke huyo limetokea siku chache baada ya
hivi karibuni, mchuna ng’ombe Musa Petro (27) naye kumuua kwa kumchinja
kwa kisu mpenzi wake, Jessica Elialinga (19).
Naye Mwenyekiti wa
Wafanyabiashara wa Maduka ya Nyama Kahama, Faraji Mohamed akiongea na
gazeti hili alisema Petro ni mfanyakazi wa Nzolela katika duka lake la
nyama (bucha) ambapo alishangaa kusikia Nzolela amemchinja mke wake kama
alivyofanya mfanyakazi wake, Petro.
Wakati tunakwenda mitamboni
habari zilizopatikana kutoka Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kahama na
kudhibitishwa na OCD George Simba zilisema mtuhumiwa huyo amekamatwa.
No comments:
Post a Comment