NEMAYAN

NEMAYAN

ROBERT

  • THE HOODS SPICK

Tuesday, January 29, 2013

JE, NI KWELI CHAI INAPUNGUZA HATARI YA MTU KUPATWA NA UGONJWA WA MOYO?



CHAI imeanza kutumiwa nchini China zaidi ya miaka 4,000 iliyopita na kwa mujibu wa historia, Mtawala Shen-Nung, katika miaka ya 2737 BC, ndiye aliyekuwa akinywa chai kwa staili ya kunywa maji ya moto ambayo yaliangukiwa kwa bahati mbaya na majani ya chai. Kuanzia wakati huo unywaji chai ulindelea kukua na kusambaa duniani kama ilivyo leo.
Kabla ya kujibu swali la makala yetu ya leo, kuna umuhimu wa kuifahama chai kwanza. Kuna aina mbili za chai- Kijani na Nyeusi (Green & Black tea), ambazo utayarishaji wake unatofautiana. Chai ya kijani hupashwa joto mara baada ya kuchumwa na haifanyiwi mchakato mwingine.
Wakati chai nyeusi hukaushwa mara baada ya kuchumwa na huachwa ipate hewa kabla ya kupashwa joto. Matokeo yake chai ya kijani na nyeusi hutofautiana hata kwa muonekano, ladha na kemikali zilizomo ndani yake. Chai ya kijani inapendwa sana katika bara la Asia wakati chai nyeusi hupendelewa zaidi katika nchi za magharibi.
Aina zote mbili za chai zina kitu kinachoitwa ‘caffeine’, dawa ambayo ina athari ya kiwango fulani katika uchangamfu wa mwili. Kiwango cha ‘caffeine’ kinachopatikana kwa kunywa kikombe kimoja cha chai, kinategemea na wingi wa chai iliyowekwa, kikombe kilichowekwa chai nyingi (strong tea) kitakuwa na kiwango kikubwa cha ‘caffeine’ tofauti na kile kilichowekwa kiasi kidogo cha chai.
Ingawa haijathibitika kisayansi kama ‘caffeine’ haina madhara kabisa kwa mtoto aliye tumboni, inashauriwa kuwa wanawake wajawazito na akina mama wanaonyonyesha, wasinywe kiwango kubwa cha ‘caffeine’, hii ina maana kwamba unywaji wao wa chai uwe ni kwa kiwango kidogo, kikombe kimoja cha chai nyepesi kwa siku.
 
CHAI NA UGONJWA WA MOYO, SARATANI
Kwa miaka mingi sasa, imekuwa ikidhaniwa kuwa unywaji wa chai unaweza kutoa kinga dhidi ya ugonjwa wa moyo. Chai inaweza kutoa kinga dhidi ya ugonjwa huo kupitia virutubisho vyenye uwezo wa kudhibiti kuganda kwa damu mwilini, kitaalamu vinajulikana kama ‘antioxidants’ ambavyo vimo kwenye chai. Virutubisho hivyo pia vina uwezo wa kupunguza hatari ya mtu kupatwa na saratani.
Kwa mujibu wa watafiti mbalimbali duniani, ushahidi uliyopo kuhusu chai, ingawa siyo mkubwa sana, unaonesha kuwa chai ina manufaa kwa ujumla kiafya, na hasa kwa moyo. Utafiti mwingi umeonesha kuwa watu wanaokunywa chai wako katika hatari ndogo ya kupatwa na ugonjwa wa moyo kuliko wasiokunywa chai.
Bila shaka, kunaweza kuwepo na sababu nyingine zinazowafanya wanywaji chai kuwa salama. Aidha ushahidi wa kwenye maabara umethibitisha kuwa virutubisho vilivyomo kwenye chai hupunguza kasi ya kuganda kwa damu kwenye mishipa ambako hatimaye husababisha ugonjwa wa moyo na hatimaye kiharusi.
Swali moja ambalo bado halijapatiwa majibu sahihi ni iwapo kuongeza maziwa kwenye chai kuna athari yoyote kiafya. Utafiti wa awali ulionesha kuwa maziwa yanaweza kuingilia uwezo wa chai wa kuipa damu kinga, lakini utafiti wa hivi karibuni umebaini kuwa maziwa hayawezi kuingilia uwezo wa virutubisho (antioxidants) vilivyomo kwenye chai kufanya kazi yake ya kulinda damu isigande. Hivyo chai na maziwa nayo ni salama tu.
Jambo la kuzingatia ni kwamba unjwaji wa chai pamoja na chakula huingiliana na upatikanaji wa madini ya chuma mwilini yanayopatikana kwenye vyakula vitokanavyo na mimea.
Watu wenye madini chuma mengi mwilini (hali inayojulikana kitaalamu kama ‘haemochromatosis), ndiyo wanaoruhusiwa kula chakula huku wakinywa na chai. Hata hivyo kiwango chako cha madini ya chuma mwilini kitakuwa kizuri iwapo utakunywa chai kati ya mlo badala ya kunywa na chakula.
Jambo lingine la kuzingatia katika unywaji wa chai ni kiwango, kwani kiwango kitakachokupa faida zilizoelezwa hapa ni kile kisichozidi kikombe kimoja kwa siku, kiwango kikizidi  sana husababisha matatizo mengine, ikiwemo suala la ukosefu wa choo (constipation).

No comments:

Post a Comment